| Taasisi ya ndoa na Sheria ya Ndoa Tanzania (9) Mgogoro kati ya Waisraeli na Wapalestina ni matokeo ya Ibrahim kuzaa na mjakazi Na Mwassa Jingi Katika matoleo matatu yaliyopita, tumeendelea kufuatilia maendeleo ya Taasisi ya Ndoa kutokea kwenye uzao wa watoto watatu wa Nuhu. Tayari tumeshaona vizazi vilivyotokana na watoto hawa na jinsi ambavyo ulimwengu wa leo ulivyogawanyika kutokana na uzao huo. Leo tutaangalia baadhi ya madhara yaliyotokana na Mzee Ibrahimu kuzaa na mjakazi Hajiri na jinsi uzao huu unavyochangia katika mgogoro wa muda mrefu, kati ya waarabu wa Palestina na Waisraeli, ambao chanzo chake ni kuvurugwa kwa maadili ya ndoa. Katika matoleo kadhaa ya mfululizo wa makala haya, nimeeleza jinsi Nuhu alivyomlaani mtoto wake Hamu, kwa sababu aliona uchi wake wakati yeye Nuhu alipokuwa amelewa chakari na hajitambui. Kutokana na laana hiyo, basi uzao wote wa Hamu ulibebeshwa laana na matokeo ya laana hiyo ni pamoja na uzao wa Hamu kuendelea kuwa watumwa kwa uzao wa wale watoto wengine wawili wa Nuhu yaani Shemu na Yafethi. Pia tuliona, kutokana na historia ya uandishi wa Biblia kuwa uzao wa Shemu, ni pamoja na familia ya Ibrahimu na baadaye taifa lote la Israeli. Kwa upande wa Hamu, uzao wake uliendelea na kufikia kwa mataifa ya Waarabu na Waafrika kwa ujumla wao, uzao ambao pia alitokea mjakazi wa Sara, yaani Hajiri, ambaye alitoka nchi ya Misri. Ushahidi wa ukweli wa unabii huo wa Mzee Nuhu ni jinsi walivyo Waafrika na Waarabu ambao, ukiacha utumwa na ukoloni uliokwishapita, lakini bado Waafrika na Waarabu wameendelea kuwa jamii duni kifikra na kimaendeleo. Huko nyuma nilishawahi kueleza kuwa Waafrika pamoja na kuwa na mali asili nyingi na hali ya hewa nzuri, lakini bado vitu hivyo havijatusaidia kutengana na umaskini. Hata pale tunapopata misaada, bado misaada hiyo imeshindwa kuwa chachu ya maendeleo yetu. Tutaendelea kutegemea uzao wa Shemu na Yafethi mpaka lini! Haijulikani. Waisraeli ambao ni uzao wa Ibrahimu kupitia Isaka ni taifa dogo mpaka leo, lakini ni tishio kwa ulimwengu wote. Katika nchi ambazo Waisraeli wamekuwepo, bado wameendelea kutamba katika nyanja zote za maendeleo, kuanzia elimu hadi sayansi.Hata katika taifa kubwa kama Marekani, Wayahudi ndio moja ya jamii ambayo watu wake wanaishi maisha ya juu. Na nchi zingine ambazo zilikaribisha Waisraeli hazijawahi kujuta. Laana kwa Hamu, haikuishia tu katika kusababisha kero za utumwa na umaskini wa mwili, bali laana hizo zimeingia mpaka kwenye misingi ya kiroho na kuleta madhara ya kiroho kwa binadamu. Upinzani wa kidini ni matokeo ya uzao wa Ibrahimu na mjakazi. Ukiacha dini ndogo ndogo nyingi zilizoko duniani leo, bado utaona kuwa laana ya Hamu imekuja kuugawa ulimwengu katika dini kuu mbili zinazopingana, yaani ukristo na Uislamu. Wakati ukristo umekuja kupitia kwa Wayahudi, Uislamu ulianzia na uzao wa Hamu kwenda kwa Ishmaeli na hatimaye Mtume Muhammad. Mpaka sasa dunia inaendelea kuonja madhara mbalimbali katika maeneo yote ya kiroho, kimwili, kiuchumi na kiusalama, kutokana na kuwepo kwa familia ya Ibrahimu katika mlengo wa kulia na kushoto. Mbali na migogoro ya kidini na kiardhi, uzao wa Ishmaeli ambao umetokana na Hamu unaendelea kuongezeka na kuimarisha uadui kati yake na uzao wa Shemu na Yafethi. Zaidi ya mtafaruku wa Mashariki ya Kati, kati ya Waisraeli na Wapalestina, laana hiyo ya Hamu inajitanua zaidi kwa kuzaa Ugaidi( terrorism), ikiwa ni mbinu mpya ya uislamu kupambana na ukristo kwa kutaka kujiondoa na unyonge wa kutawaliwa kifikra zaidi. Chuki kubwa iliyoko kati ya ulimwengu wa kiarabu ukiungwa mkono na ulimwengu wa kiislamu dhidi ya mataifa ya Magharibi, mara nyingi huchukuliwa kuwa ni matokeo ya sera mbaya za nchi za Magharibi zikiongozwa na Marekani, lakini ukweli ni kwamba chuki hiyo chanzo chake ni uzao wa watoto wa Ibrahimu, yaani mtoto wa muungwana - Isaka na mtoto wa mjakazi - Ishmaeli. Ni vema tupitie maandiko ya Biblia kwa ufupi ili kutoa picha halisi ya hayo ambayo nimeyaeleza mpaka sasa. “Mtoto akakua, akaachishwa kunyonya; Ibrahimu akafanya karamu kuu siku ile Isaka alipoachishwa kunyonya. Sara akamwona yule mwana wa Hajiri Mmisri, ambaye alimzalia Ibrahimu, anafanya dhihaka. Kwa hiyo akamwambia Ibrahimu, mfukuze mjakazi huyu na mwanawe, maana mwana wa mjakazi hatarithi pamoja na mwanangu, Isaka. Na neno hilo lilikuwa baya sana machoni pa Ibrahimu, kwa ajili ya mwanawe. Mungu akamwambia Ibrahimu, neno hili lisiwe baya machoni pako, kwa ajili ya huyo mwana, na huyo mjakazi wako. Kila akuambialo Sara, sikiza sauti yake, kwa maana katika Isaka uzao wako utaitwa. Naye mwana wa mjakazi nitamfanya kuwa taifa, maana huyu naye ni uzao wako”, (Mwanzo 21:8-13). Maandiko haya yanatupa mitazamo tofauti kati ya Sara, Ibrahimu na Mungu. Kusema kweli tangu mwanzo Ibrahimu alimpenda Ishmaeli mtoto wa mjakazi kama mtoto wake na wala hakutegemea kuwa itatokea vinginevyo. Sara naye baada ya ile ahadi ya kumzaa Isaka kutimia, hakuona haja tena ya kuwa na mjakazi wake pamoja na mtoto wake Ishmaeli. Kutokana na maandiko hayo hapo juu, inaonesha kuwa kulikuwa kutokupendana kwa watoto hao wawili, na hasa Ishmaeli kumchukia Isaka. Kwa hiyo, Sara alimtaka mume wake Ibrahimu kumfukuza mjakazi na mtoto wake, kwa sababu ya kuona mtoto wake Isaka anateswa na mtoto wa mjakazi na kwamba lile hitaji lake la kutaka mtoto wa kurithi tayari halikuwepo kwa sababu Isaka tayari alishazaliwa. Mzee Ibrahimu hata hivyo, hakuwa tayari kumfukuza mjakazi na mtoto wake, kwa sababu yeye alimhesabia Ishmaeli sawa kabisa na Isaka. Yeye aliona kuwa wote, yaani Isaka na Ishmaeli ni watoto wake na kwa hiyo hakuona sababu ya kutenganishwa. Mungu aliamua kuingilia kati mjadala wa Ibrahimu na Sara na kumtaka Ibrahimu akubaliane na hoja ya mke wake ya kuwafukuza Hajiri na mtoto wake. Kwa hiyo Ibrahimu alikubaliana na hoja ya mke wake na hivyo akamfukuza mjakazi wake na mtoto. Kwa nini Mungu awatenganishe Isaka na Ishmaeli? Hili ni swali la msingi, ingawa ni swali gumu. Kwa akili ya kibinadamu, tusingetegemea Mungu akubaliane na hoja ya Sara, ya kutaka mjakazi wake pamoja na mtoto wafukuzwe. Tena baya zaidi ni kwamba walifukuzwa wakiwa hawajui pa kwenda, tena katika mazingira magumu ya jangwa. Kwa nini Mungu ambaye ni mwenye huruma na upendo akubaliane na hoja ya kufukuzwa kwa Hajiri na mtoto wake? Bila shaka, Mungu alijua tatizo ambalo lingetokea siku za mbeleni. Aidha, kwa upande mwingine tunaweza kuchukulia tu kwamba ule ulikuwa ni wivu Sara kutaka mtoto wake tu ndiye arithi. Kama Ishmaeli akiwa bado mtoto mdogo tayari alishaanza kumchukia mdogo wake Isaka, je hali ingekuwaje kama wote wawili wangeendelea kukua pamoja kama familia moja ya Mzee Ibrahimu? Kwa vyo vyote vile lazima kungekuja kuwa na tatizo kubwa kuliko hata lile la kufukuzwa kwa Hajiri na mtoto wake. Inawezekana hata lile lililotokea kwa familia ya Adamu, ambapo Kaini alimuua ndugu yake lingetokea. Lakini tukirejea nyuma utakumbuka kuwa Mungu alimwambia Ibrahimu kuwa mrithi wake angetokana na yeye na mkewe Sara. Kama Isaka na Ishmaeli wangekua pamoja, ilikuwa pia lazima wote wawili warithi pamoja. Na pili jina la Ibrahimu lingeendelezwa kutokana na uzao wa Isaka na Ishmaeli na hivyo kuchanganyika kwa uzao wa Hamu na Shemu kinyume na maagizo ya laana ya Mzee Nuhu. Ingawa Ibrahimu alishasahau hiyo, Mungu hakusahau. Swali lingine ambalo tunaweza kujiuliza nalo ni hili; kuna dhambi gani au kosa gani mtoto wa Sara (muungwana) kurithi pamoja na mtoto wa mjakazi? Kimsingi, hoja ya kuwa mtoto wa muungwana hatarithi na mtoto wa mjakazi ilitoka kwa Sara ingawa ilikuwa na msingi wa kiroho pia na ndiyo maana Mungu naye akaiunga mkono. Je, Mungu ana ubaguzi? Hii ndiyo hoja kubwa miongoni mwa jamii ya kimataifa kuhusu mgogoro kati ya Wapalestina na Waisraeli, ambapo karibu dunia yote wanaona kuwa sio kweli kuwa Mungu kwa namna moja au nyingine ahusike na ubaguzi unaoendelezwa na wayahudi na wapalestina leo, ikiwa na maana kuwa baadhi ya watu kama wayahudi, Mungu awape upendeleo maalumu tofauti na tabia yake kuwa yeye si Mungu wa upendeleo. Ni kweli Mungu hana upendeleo, isipokuwa, mwanadamu ndiye anayechagua mwelekeo wake wa baadaye, kutokana na hiari yake ya kutumia akili na kufanya maamuzi. Uchaguzi wa mwanadamu katika njia zake ndio unaoweza kumfanya Mungu aonekane ni mbaguzi. Huko nyuma tumeona kuwa Mungu alikubaliana na laana ya Nuhu kwa mtoto wake, vinginevyo hiyo laana isingempata Hamu. Lakini Mungu aliidhinisha laana hiyo kwa sababu ya kitendo cha Hamu, ambacho kilikuwa kinyume cha maadili. Kama Mungu angeruhusu mtoto wa mjakazi arithi pamoja na mtoto wa muungwana (Isaka), basi ingekuwa anaunganisha tena uzao wa watoto wa Nuhu kuwa na mazingira yanayofanana. Hiyo nayo bila shaka ingesababisha madhara makubwa kwa kizazi cha binadamu mapema zaidi kuliko ilivyotokea kwa Isaka na Ishmaeli. Mungu alichofanya ni kuchukua hatua ya makusudi za kumsaidia Hajiri amlee mtoto wake, na yeye kuahidi kuwa Ishmaeli naye angekuwa taifa kubwa. Mpaka leo vizazi vya Isaka na Ishmaeli ndivyo vinavyougawa ulimwengu wa leo katika fikra na mtazamo tofauti tofauti kidini na kisiasa. Ulimwengu wa uzao wa Ishmaeli umeendelea kukua kidini na kisiasa, ukishindana na ule ulimwengu uliotokana na watoto wale wengine wawili wa Mzee Nuhu. Mbali na laana ya Hamu, ambayo iliuweka uzao wake chini ya utumwa, bado uzazi wa Ibrahimu na mjakazi wake nao uliendeleza kuifanya hali iwe mbaya zaidi, sio tu kuwa na watu bora (superior) na duni (inferior), lakini hali hiyo imeongeza uadui kati ya uzao wa Isaka na Ishmaeli, kama ambavyo mgogoro wa Mashariki ya kati ulivyo. Mgogoro huo una sura zote mbili, kisiasa na kidini. Mtume Paulo naye amejaribu , kwa neema ya Mungu, kuchambua sababu za mtoto wa mjakazi kutokurithi pamoja na mtoto wa muungwana. Hivyo ndivyo anavyosema. “Kwa maana imeandikwa ya kuwa, Ibrahimu alikuwa na wana wawili, mmoja kwa mjakazi, na mmoja kwa muungwana. Lakini yule wa mjakazi alizaliwa kwa mwili, yule wa muungwana kwa ahadi. Mambo haya husemwa kwa mfano; kwa maana hawa ndio kama maagano mawili, moja kutoka mlima Sinai, lizaalo kwa utumwa, ambalo ni Hajiri. Maana Hajiri ni kama mlima Sinai ulioko Arabuni, umelingana na Yerusalemu wa sasa; kwa kuwa anatumika pamoja na watoto. Bali Yerusalemu wa juu ni muungwana, naye ndiye mama yetu sisi…..Basi, ndugu zangu, kama Isaka sisi tu watoto wa ahadi. Lakini kama vile siku zile yule aliyezaliwa kwa mwili alivyomwuudhi yule aliyezaliwa kwa Roho, ndivyo ilivyo na sasa. Lakini linasemaje andiko? Mfukuze mjakazi na mwanawe, kwa maana mwana wa mjakazi hatarithi kabisa pamoja na mwana wa muungwana. Ndiposa, ndugu zangu, sisi sio watoto wa mjakazi, bali tu watoto wa huyo aliye muungwana (Wagalatia 4:21-31). Ni kutokana na uzazi wa muungwana, yaani Sara mke wa Ibrahimu ndio ulimwengu ulikuja kupata mkombozi,Yesu Kristo. Tunajifunza nini na nadharia hii ya mtoto wa muungwana na mtoto wa mjakazi au mtumwa? Nadharia hii ina uhusiano mkubwa na maendeleo ya Taasisi ya Ndoa na kizazi cha binadamu. Pale ambapo wanadamu wanaishi na kuzaliana kwa kufuata misingi ya ndoa kama ilivyowekwa na Mungu, basi uhusiano wa Mungu na kizazi hicho huwa mzuri na maendeleo ya binadamu huendelea kupata kibali kwa Mungu. Mazingira ya ndoa yana mchango chanya au hasi katika maendeleo ya kimwili au kiroho, kwa binadamu kutegemeana na ubora wa ndoa yenyewe, kama inafuata misingi sahihi au la. |