Taasisi ya Ndoa na Sheria ya Ndoa Tanzania (10)
Mwendelezo wa ndoa katika kizazi cha Ibrahimu
Katika matoleo kadhaa yaliyopita ya makala haya, tumekuwa tukifuatilia uendelezwaji wa misingi halisi ya ndoa
kama ilivyowekwa na Bwana Mungu mwenyezi. Na msingi mkubwa ambao kila mwanadamu anapaswa
kuuangalia na kuuheshimu ni ule wa “mume mmoja kwa mke mmoja”. Huko nyuma tuliona kuwa uzao ambao
ulikiuka msingi huu ni ule ambao ulimwasi Mungu.Uzao ambao ulizingatia misingi ya ndoa, Mungu aliendeleza
uhusiano na kizazi hicho.

Tumeona pia  kwamba kuyumba kwa familia ya Ibrahimu kulisababishwa na familia hiyo kuamua kupata mtoto
kupitia mjakazi wao na madhara ya kuzaliwa kwa Ishmaeli yapo mpaka leo, yaani uadui kati ya wayahudi na
wapalestina. Mambo hayo kwa ufupi yanatuonesha madhara ya kukiuka misingi ya ndoa. Hata leo hii madhara
yanayozikumba familia nyingi katika dunia hii kwa kiasi kikubwa hutokana na kuishi kinyume na matakwa ya
misingi ya ndoa.

Tuangalie ndoa ya Isaka

Kabla ya Mzee Ibrahimu kufariki dunia, aliona ni vema mtoto wake wa pekee aliyempata kwa muujiza Isaka  
aendeleze uzao sahihi kwa kupata mke sahihi kutoka kwa familia bora. Tunasoma hivi:”Basi Ibrahimu alikuwa
mzee mwenye miaka mingi, na Bwana alikuwa amembariki Ibrahimu katika vitu vyote. Ibrahimu akamwambia
mtumishi wake, mzee wa nyumba, aliyetawala vitu vyake vyote…………. Tafadhali uutie mkono wako chini ya
paja langu, nami nitakuapisha kwa Bwana Mungu wa mbingu na Mungu wa nchi kwamba hutamtwalia
mwanangu mke katika binti za wakanaani ambao nakaa kati yao, bali enenda hata nchi yangu, ukamtwalie
mwanangu mke (Mwanzo 24:1-4).

Ibrahimu kama tunavyojua aliondolewa katika familia yake na kuambiwa aende katika nchi ambayo ni ya ukoo
wa Hamu, yaani uzao wa mtoto wa Hamu aliyeitwa Kanaani, na watu waliotokana naye waliitwa wakaanani.
Kwa kufuatilia ukoo wa watoto watatu wa Nuhu, bado Ibrahimu na wakanaani walikuwa karibu tu kama ndugu.
Lakini kwa nini hakutaka mtoto wake apate mke kutoka kwa watu aliokuwa anaishi nao, yaani wakanaani
ambao walitokana na kizazi cha Hamu?

Ibrahimu alijua fika kuwa hao hawakuwa watu sahihi kwa kutwaa mke sahihi. Mzee Ibrahimu kwa kujua
ulazima wa ndoa sahihi kwa maendeleo ya kizazi cha mtoto wake, hakulichukulia suala la mtoto wake Isaka
kupata mke kwa mizaha.

Ibrahimu pamoja na uzee wake huo bado aliendelea kumheshimu Mungu kama ilivyokuwa wakati mwingine
wowote. Na kutokana na uchaji Mungu wake, pia alitambua umuhimu wa mchango wake kwa ndoa ya mtoto
wake Isaka, kabla ya kufa kwake. Alijua kuwa mke mwema hupatikana katika familia inayomjua Mungu. Mzee
Ibrahimu alijua ulazima wa mtoto wake kupata mke kutoka kwa familia aliyokuwa anaijua, ingawa  
hakumfahamu yule binti ambaye angekubali kuwa mke wa mwanawe Isaka.

Ili kuhakikisha mtumishi wake hafanyi kinyume na maagizo yake,  Mzee Ibrahimu aliamua kumwapisha
mtumishi wake  kwa Mungu ili mtumishi huyo akivunja kiapo hicho apate madhara yeye mwenyewe. Kule
kumwapisha mtumishi wake kunaonesha ni kwa kiasi gani Mzee Ibrahimu alijua umuhimu wa mtoto wake
kupata mke sahihi.

Kwa wale waliobahatika kusoma makala niliyoandika kuhusu “Ulimwengu wa wasioolewa” iliyotoka katika
ukurasa huu mwaka jana, bila shaka watakumbuka jinsi nilivyotumia sura hii ya 24 ya kitabu cha Mwanzo
kuainisha kanuni nne za lazima kwa watu wanaotaka kuingia kwenye ndoa kuzifuata.

Ninachotaka kueleza hapa kwa ufupi ni kwamba historia hii ya watu wa Biblia -Ibrahimu na Isaka inatuonesha
jinsi watu hao walivyofuata misingi ya ndoa, na kwa kufanya hivyo vizazi vyao viliendelea vema kwa kudumisha
uhusiano wao na Mungu, hatua ambayo ilisaidia pia kwa ustawi wa maisha yao kimwili na kijamii.
Ndoa ni kiini cha familia na taifa bora, ndiyo maana tunasisitiza kufuatwa kwa kanuni na misingi yake
kikamilifu. Tunaona kuwa mtumishi wa Mzee Ibrahimu alifuata maagizo ya bwana wake na kufanikiwa kupata
mke mwema kwa ajili ya Isaka.

Mungu alivyolinda ndoa za Ibrahimu na Isaka

Ndoa kati ya Ibrahimu na Isaka zilipata baraka na ulinzi kamili wa Mungu, hata pale kulipokuwa na tishio la
kuzivunja  kutoka nje. Ukisoma sura za ishirini na ishirini na saba za kitabu cha Mwanzo, utaona jinsi ambavyo
Ibrahimu na Isaka walivyokutana na matishio ya kunyang’anywa wake zao na Mfalme Abimeleki kwa nyakati
tofauti.
Ingawa wao wenyewe hawakuwa na uwezo wa kuwalinda wake zao katika mazingira magumu ya njaa wakiwa
ugenini, lakini Mungu aliweza kuwatetea na kuwalinda wake zao wasiporwe na watu wengine pale ambapo
wao (Ibrahimu na Isaka), walikuwa tayari kuwaachia ili wasiuawe na Mfalme Abimeleki au watu wengine
ambao wangetamani wake zao.
Biblia inasema Sara na Rebeka walikuwa ni wanawake wazuri wa uso na kwa hiyo watu wengine na hasa
wafalme wangeweza kuwanyang’anya au kuwaua wao ili wawapate wake zao. Hii ndio faida kubwa ya kuwa na
uhusiano na Mungu, kwani Mungu anakuwa mhusika namba moja katika kuzuia ndoa kusambaratika pale
ambapo familia inaweza kupitia mikikimikiki ya maisha.

Je! Hali ingekuwaje kama Ibrahimu na Isaka wasingefuata maadili na misingi ya Mungu katika kujenga ndoa
zao? Bila shaka yoyote Mungu asingehusika kabisa katika ulinzi wa wake zao na familia zao kwa ujumla.
Ingawa Ibrahimu na Sara, Isaka na Rebeka hawakupata watoto wengi katika ndoa zao, lakini polepole Mungu
aliendeleza vizazi vyao na  hatimaye kuwa taifa na mataifa kama  Mungu alivyomwapia Ibrahimu tangu mwanzo.

Ingawa maisha ya Ibrahimu yanaonekana kuwa ya matatizo kindoa, lakini kusudi la Mungu lilitimia. Kama
Ibrahimu babaye, hata uzao wa Isaka nao ulikuwa wa matatizo. Mke wa Isaka, Rebeka naye kama mama   
mkwe wake, alikuwa tasa. Bado hali hiyo haikumwondoa Isaka katika kumtumaini Mungu. Isaka kwa sababu
alimjua Mungu, alimwomba Mungu ampe uzao. “Isaka akamwomba Bwana kwa ajili ya mke wake, maana
alikuwa tasa. Naye Bwana akamwitikia na Rebeka mkewe akachukua mimba, (Mwanzo 25:21).

Uhusiano mzuri kati ya mtu na Mungu utamsaidia katika mambo mengi, ikiwa ni pamoja na yale ambayo
hayawezekaniki kwa uwezo wa kibinadamu. Isaka hakufikia kutafuta ufumbuzi nje ya mapenzi ya Mungu. Kwa
mtu mwingine asiyemjua Mungu, kutokupata mtoto ni jaribu tosha la kumwondoa katika imani. Lakini tunaona
Isaka alipoona mke wake hazai hakufikiria kuoa mke mwingine, bali alimwomba Mungu na Mungu alimwitikia.
Huku ndiko kuendeleza misingi ya ndoa, kwa sababu ndoa ni taasisi aliyoianzisha Mungu, ataendelea siku
zote kuhakikisha kuwa wale wote wanaoiheshimu na kuifuata misingi ya ndoa, maisha yao yanafanikiwa, ikiwa
ni pamoja na kuendelea kupata uzazi halali.

Kumbuka ni Mungu ndiye aliyesema watu wazae na kuongezeka. Je, ataachaje kuhusika na masuala ya ndoa
na familia, wakati ndiye aliyeanzisha familia na ndoa ya kwanza? Mungu anaheshimu ndoa kuliko watu
wanavyofikiria. Kama wanadamu wataendelea kumtii Mungu katika kufuata misingi ya ndoa, Mungu naye
ataendelea kuwasikia, hata pale matatizo yanapojitokeza katika ndoa na familia zao.

Siku hizi, na hasa vijana hawana tena imani kwa Mungu kuhusu maisha ya ndoa na familia. Vijana wa leo
hudiriki hata kufikiria kuwa na mahusiano ya kindoa (kufanya ngono), kabla ya ndoa kwa sababu tu za
kibinadamu, na moja ya sababu  kubwa ikiwa ni kupima uwezekano wa mwanamke kuzaa. Katika makanisa
mengi ya kidini, ndoa nyingi hufungwa kanisani, watu wakiwa tayari wameshakuwa familia kwa kuishi pamoja,
wengine huwa tayari ni wajawazito wakati wa kufunga ndoa. Hii kwa vijana huwa ndio ushahidi wa kile
wanachofikiria kuwa ni vema kujua kama mke ana uwezo wa kuzaa au hapana, kabla ya kuingia kwenye
mkataba wa ndoa.

Mchezo huu, ingawa unaweza kuonekana kuwa una mantiki kibinadamu, lakini upo nje ya misingi ya ndoa.
Isaka aliletewa mke na wala hakuletewa  yule mke kwa majaribio. Kama Isaka angekuwa na akili kama za
vijana wa leo, maana yake angemrudisha Rebeka kwao pale alipochelewa kuzaa. Isaka kwa sababu alipata
mke kwa taratibu zote halali na za ki-Mungu, hakuwa na shaka yoyote hata alipogundua kuwa mke wake ni
tasa. Alijua utasa huo ni tatizo dogo kwa Mungu, kwa sababu ni Mungu ndiye aliyehusika katika kumpatia huyo
mke. Kama taratibu zilizotumika kumpatia Isaka mke hazikumhusisha Mungu, Isaka asingekuwa na ujasiri
hata wa kumkaribia Mungu, pindi mke wake alipoonekana kuwa tasa. Lakini kwa sababu alikuwa na uhakika
kuwa huyo mke amempata kwa njia na taratibu halali, ndio maana alikuwa na ujasiri wa kumwomba Mungu
aingilie kati na kuvunja utasa wa mke wake.

Angalizo kwa  vijana

Ni vema vijana wetu wa leo na hasa wale waliokwisha kutoa maisha yao kwa Yesu Kristo, kutokuwa na
wasiwasi wowote katika kufikiria maendeleo ya familia na hasa suala la kupata au kutokupata watoto baada ya
ndoa. Maisha ya Ibrahimu na mwanawe Isaka yanatosha kabisa kuwa ushahidi na kielelezo  kuwa maisha ya
ndoa yapo mikononi mwa Mungu, kwa sababu yeye Mungu ndiye mwanzilishi wa Taasisi ya Ndoa.

Jambo la msingi kwa kila kijana wa kiume kuzingatia ni kufuata misingi, kanuni na taratibu zilizoainishwa katika
Biblia wakati wa kutafuta mke. Mara baada ya kupata mke kwa kufuata taratibu zote za ki-Mungu, hakuna tena
sababu yoyote ya kuwa na shaka juu ya uzazi wa mke wako.  Kama mazingira au matatizo ya kuchelewa kupata
mtoto kama ilivyotokea kwa Ibrahimu na Isaka yatatokea,  basi Mungu yule wa Ibrahimu na Isaka ndiye Mungu
wako leo na kwa kiwango kile alichowasaidia Ibrahimu na Isaka kuondoa  matatizo ya familia zao, ndivyo
atakavyofanya hata kwako leo. Mungu habadiliki na ahadi zake ni za kweli. Kila anayemtumaini hatatahayarika.
MAKALA ILIYOPITA YA 9
Jisomee makala ili uelimike na kupanua
ufahamu