Je, ni kweli Serikali ya awamu ya nne ina udini?
Na Sakofu Sylvester Gamanywa
Zimekuwepo hisia miongoni mwa baadhi ya madhehebu ya Kikristo kwamba Serikali ya awamu ya
nne imeanza kuonesha udini katika utendaji wake. Kigezo kikuu kinachotumiwa katika madai haya  
ni kuteuliwa kwa waislamu wengi kushika madaraka ya uongozi wa juu. Hofu iliyotawala miongoni
mwa waliotawaliwa na dhana hii ni tafsri kwamba huu ni mkakati maalum wa kuweka waislamu
wengi madarakani ambao hatimaye wataifanya Tanzania iwe nchi ya Kiislamu. Je! Hivi ni kweli
Serikali ya sasa imejaa udini? Vigezo vinavyotumika kueneza uvumi huu vina mantiki? Je! Hivi ni
haki na halali kuanza kumshutumu Rais ati kwa sababu kuna idadi  kubwa ya Waislamu katika
Serikali yake? Hoja hii imedhamiria kujibu maswali haya na mengineyo muhimu kwa nia ya
kujipanga upya kimtazamo:

Si jambo rahisi kuifanya Tanzania nchi ya Kiislamu

Nimeamua leo kuleta hoja hii nyeti kwa sababu nimekuwa nikisumbuliwa na baadhi ya wakristo wenzangu, hususan
viongozi wa madhehebu ya Kikristo, wakitaka kuniaminisha kwamba Serikali ya awamu ya nne ina udini. Aidha, baadhi
yao wamenikumbusha mambo ya zamani ya mikakati ya OIC na IAO ilivyowahi kuitikisa nchi yetu kisiasa. Kwa kuwa mimi
mwenyewe nimekuwa mwanaharakati wa siku nyingi wa kutetea juhudi za kudumisha amani na utulivu, pamoja na uhuru
wa kuabudu kwa kila dini katika jamii; nimeanza kushinikizwa kuendeleza uanaharakati  wangu kuhusu madai waliyo
nayo dhidi ya uteuzi wa watendaji wa Serikali ya awamu ya nne.

Kwa hiyo basi, kupitia makala haya, napenda kwanza kuwaondolea wasiwasi na hofu wakristo wenzangu msikubali
kujiruhusu kutawaliwa na hisia za jinsi hii katika jamii. Nasema hivi kwa sababu, hata kama huko zamani ziliwahi kuwepo
dalili za udini katika baadhi ya watendaji wa Serikali zilizopita, tusisahau kwamba hivi sasa mambo mengi yamebadilika
sana, tena ghafla. Hizi ni enzi mpya za utandawazi ambamo kila kitu si siri tena. Kwa kadri mwingiliano wa kijamii kutoka
nje unavyozidi kuongezeka, ndivyo hata fikra za kujaribu kuifanya Tanzania iwe nchi ya kidini pia zinazidi kufifia kama
sio kufa kabisa.

Baada ya maelezo yangu hapa juu, ningependa kutahadharisha mapema kwamba, madai kwamba kuteuliwa waislamu
wengi kushika madaraka ni dalili za kutaka kuifanya Tanzania iwe nchi ya Kiislamu, si sahihi. Mtazamo wa jinsi hii si
mzuri, hususan kwa wakristo wenzangu. Sote ni mashahidi wa kweli kwamba nchi hii imekuwa ikiongozwa kwa misingi ya
Katiba. Kila Mtanzania anafahamu bayana kwamba, Serikali ya Nchi ni ya kisekula (Secular State); kwa maana kwamba
Serikali haina dini wala haipo kupendelea dini moja dhidi ya nyingine.

Kwa hivyo basi, nazidi kusisitiza kwamba si tafsiri sahihi kudai kwamba Rais ameteua watendaji wakuu serikalini kwa
misingi ya udini. Ninaamini kwamba uteuzi wa Rais wetu umezingatia zaidi uwezo wa mtu na si dini anakotoka. Rais wetu
si mgeni na hisia hizi za udini. Anafahamu kabisa kwamba hisia kali za udini kama zikiendekezwa hatimaye zinaweza
kutupeleka mahali pabaya. Wala hawezi kuthubutu kufanya makosa kama haya hapa mwanzoni mwanzoni tu wa
utawala wake.

Ni mapema sana kuhukumu mambo

Hapa napenda kukumbusha kwamba Wakristo tunajulikana kwa utamaduni wa kutumia hoja katika kusema, badala ya
kutawaliwa tu na hisia za jazba na tafsiri zisizothibitishwa.

Kwa busara zile zile, lazima tukubali kwamba hivi sasa ni mapema mno kuwahukumu walioteuliwa kabla hata
hawajaanza kufanya kazi zenyewe walizoteuliwa kufanya. Lazima tuwape uhuru na nafasi walioteuliwa kuongoza nchi
waoneshe uwezo wao.

Nimeambiwa kwamba mkakati wa Waislamu kuwa wengi katika utawala ni wa kutaka kubadili Katiba ya Nchi na kuweka
vipengele vya upendeleo wa kidini kwa dini moja dhidi ya dini nyingine. Na kwa sababu wao tayari watakuwa ni wengi
wakati wa kupiga kura; basi agenda yao itapita bila kupingwa, kwa kisingizio cha Demokrasia. Hizi ni hisia kali sana za
kidini na zisipodhibitiwa zinatishia amani na utulivu wa taifa letu.

Bado napinga kwa kusema hisia hizi si sahihi kwa sababu bado hakuna ajenda ya kubadili Katiba iliyowasilishwa
bungeni yenye mwelekeo wa kuifanya Serikali ivunje utamaduni wake wa kuwa ya kisekula kama ilivyo hivi sasa. Na
kama ipo inakuja, basi tuisubiri ijitokeze.

Narejea kusema tena kwamba si busara za Kikristo kuanza kueneza uvumi mitaani kwamba sasa tumeanza kutawaliwa
kidini, kwa kuwa viongozi wa ngazi za juu wengi wao ni Waislamu. Tusubiri tuuone udini huo kama upo kweli, ukijitokeza
kwa vitendo. Ni muhimu kuwa na ushahidi kamili ndipo tuseme.

Tusikubali kueleweka vibaya kuwa sisi ndio wenye udini

Napenda pia kuchukua fursa hii kutahadharisha juu ya dhana kwamba waislamu wengi wakiteuliwa kushika madaraka
badala ya wakristo ni udini kwa upande mmoja; kisha tukasahau kwamba mtazamo huu unaweza kutafsiriwa vibaya
dhidi yetu kwamba nasi tumeanza kuonesha udini! Kama tutaendelea kuwatazama watendaji wanaoteuliwa na Rais kwa
‘jicho la dini’ wanakotoka; tayari nasi tutakuwa tumeangukia upande wa udini dhidi ya Waislamu!

Lazima tukubali mabadiliko. Kama tutaendelea kufikiri kwamba wakristo wengi kutawala ndiko kutaifanya Tanzania isiwe
nchi ya kidini; nadhani tutakuwa tumekosea kimtazamo. Maana wasio Wakristo nao wataendelea kutafsiri kwamba
Tanzania ni nchi ya Kikristo, ati kwa sababu akina Mathayo na Yohana ndio waliojaa madarakani kuliko Issa na Yahaya.

Tukumbuke kwamba huko nyuma yaliwahi kuwepo madai kutoka baadhi ya vikundi vya Kiislamu vikishinikiza tafsiri  
kwamba Tanzania ni ‘nchi ya Kikristo’,  ati kwa sababu wakristo wengi ndio waliojaa madarakani kuliko Waislamu. Sisi
nasi tukawa tunajitetea kwa hoja kwamba wakristo wengi  huwepo madarakani kutokana na uwezo wao na si kwa
sababu ni wakristo. Tukatafsiri kwamba wenye madai ya jinsi hii wana udini.

Haya sasa, idadi ya Waislamu inapoongezeka katika utawala kuliko ilivyokuwa huko zamani, baadhi yetu tumeangukia
katika mtego ule ule wa kutafsiri kuwa huu ni udini. Tusipojirekebisha tayari tutawapa nguvu wasio wakristo ‘kutubatiza’
jina la ‘udini,’ hali ambayo hata kama tulikuwa na hoja za msingi tutapuuzwa. Tutaitwa ‘Mujahidina wa Kikristo’! Sidhani
kama huko ndiko tunakotaka kwenda.
Itaendelea toleo lijalo.